CONSTITUTION



KATIBA YA CHAMA CHA MSHIKAMANO NA
MAENDELEO YA NKUNGI NA VIJIJI JIRANI
KATIKA WILAYA MPYA YA MKALAMA, MKOANI SINGIDA
YA JAMII INAYOISHI DAR ES SALAAM
(Toleo la Pili)


1)   UTANGULIZI
Ili kuimarisha umoja wa wanajamii wa Nkungi na Vijiji Jirani vya Nduguti, Nkalakala, Mwando, Mwanga, Kidarafa, Mng’anda, Malaja, Singa, Ilunda, na Iambi  katika wilaya mpya ya Mkalama waishio Dar Es Salaam, tumeamua kwa hiari na kwa dhati bila kulazimishwa na mtu yeyote kuanzisha Kikundi cha Umoja wetu yaani CHAMA.

2)   JINA LA CHAMA 
Jina la Chama litakuwa Mshikamano na Maendeleo ya Nkungi na Vijiji Jirani ya Jamii Inayoishi Dar Es Salaam (kwa kifupi: Kwilae Social Development Group). Jina Mshikamano na Maendeleo lina maana ya kushirikiana kwa dhati kama familia moja inayoishi Dar Es Salaam kwa shida na raha, yaani kuwa na umoja unaofungamana kwa dhati unaoudumisha upendo,ushirikiano, kufarijiana na pia kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Jamii inayoishi Nkungi na Vijiji Jirani katika wilaya ya Mkalama mkoani Singida. Anwani ya chama itakayotumika itakuwa kama ifuatavyo: Private Bag 70612, DAR ES SALAAM.

3)   MADHUMUNI YA CHAMA
a)    Kuwa na Mfuko utakaosaidia wanachama kuwa na mshikamano,
b)   Kuunganisha wanajamii wa Nkungi na Vijiji Jirani waishio Dar Salaam;
c)    Kutoa msaada utakaoidhinishwa kwa mwanachama ambaye amepatwa na msiba au kuumwa sana;
d)    Kushiriki katika shughuli za maendeleo ya Nkungi na Vijiji Jirani kama zitakavyopitishwa na jamii hiyo.

4)   SIFA ZA MWANACHAMA
a)    Ni yule ambaye anaipenda kwa Dhati Nkungi na Vijiji Jirani;
b)   Awe na umri usiopungua miaka kumi na nane (18);
c)    Ni yule ambaye anajitegemea na ana akili timamu;
d)    Ni yule ambaye anaishi Dar Es Salaam na ambaye wazazi/ ndugu zake wanaishi Nkungi na Vijiji Jirani;
e)    Ni yule ambaye anaweza kusoma na kuandika. Awe tayari kuielewa, kuitetea na kutekeleza masharti yote ya uanachama;
f)     Ni yule ambaye anaishi nje ya Dar Es Salaam na amependa kuendelea kuwa mwanachama kwa kutimiza masharti yote ya chama yaliyomo kwenye Katiba;
g)    Yule anayetoka nje ya Dar Es Salaam na anatoka katika vijiji husika (Aya Na. 1).

5)   HAKI ZA MWANACHAMA
a)    Kushiriki kikamilifu katika awamu zote za uchaguzi wa viongozi wa chama;
b)   Kupata huduma za umoja kama ilivyoainishwa katika Katiba;
c)    Kuwania kuchaguliwa katika nafasi yoyote ya uongozi wa chama isipokuwa mwanachama anayeishi nje ya Dar Es Salaam;
d)    Kutoa mapendekezo, malalamiko au kudai mabadiliko ili kudumisha chama. Atafanya hivyo kwa maandishi na kuyafikisha kwa Katibu wa Chama.
e)    Kujua maendeleo ya chama;
f)     Kuidhinisha mipango na bajeti ya chama; na
g)    Kuomba kujitetea endapo amefanya kosa, kusimamishwa au kufukuzwa uanachama au uongozi ili kuondolewa au kupunguziwa adhabu.

6)   MAPATO YA CHAMA
Mapato ya Chama yatapatikana kwa njia zifuatazo:
a)    Hisa za kila mwanachama kwa mwaka;
b)   Ada ya kila mwezi;
c)    Michango ya rambirambi;
d)    Ruzuku; na
e)    Michango mbalimbali kama itakavyopitishwa na wanachama.

7)   KUJIUNGA NA CHAMA
Ili kukiwezesha Chama kufanya kazi zake ipasavyo, kila mwanachama atalazimika kuchangia Mfuko wa Chama kama ifuatavyo:
a)    Kujaza fomu maalum ili kujiunga na Chama kwa shilingi 5,000/=; na
b)   Kulipa kiingilio cha  uanachama shilingi 100,000/= (laki moja) kama hisa.

Hata hivyo, viwango hivyo vya michango vinaweza kubadilika kulingana na mahitaji ya wakati husika. Mapato hayo yatawekwa katika Akaunti Maalum itakayofunguliwa kwenye Tawi la Benki linaloruhusu kutoa kiasi kinachoweza kukidhi mahitaji yanayokusudiwa na wanachama.

8)   UTUNZAJI WA FEDHA ZA CHAMA
a)    Fedha za Chama zitatunzwa katika Benki iliyochaguliwa na wanachama. Fedha za Chama zitatolewa benki kwa idhini ya wajumbe walichagulia na wanachama;
(i)   Mhasibu;
(ii)  Katibu;
(iii) Katibu Msaidizi; na
(iv) Mjumbe aliyechaguliwa.
b)   Benki statement ya akaunti ya Chama itawasilishwa katika Mkutano Mkuu kwa uchambuzi kila baada ya miezi mitatu;
c)    Hesabu za Chama zitakaguliwa kila baada ya miezi mitatu (3) na taarifa kuwasilishwa katika kikao cha pamoja kati ya kamati ya usalama na kamati ya utendaji;
d)    Taarifa ya ukaguzi na maoni ya kamati ya utendaji itawasilishwa na kuthibitishwa na Mkutano Mkuu;
e)    Taarifa itakapokubaliwa na mkutano mkuu itasainiwa;
f)     Ili kuwawezesha wanachama kiuchumi katika siku za usoni, Chama kitatafakari kwa kina namna ya kuwawezesha wanachama kiuchumi; na
g)    Endapo Kamati ya Usalama itathibitisha kwamba fedha za Chama zimepotea, mhusika au mtunza hazina atazirudisha haraka kwa mujibu wa kanuni za Chama la sivyo michango yake itafidia upotevu huo.Endapo kiasi kilichoibiwa ni kikubwa ikilinganishwa na akiba ya mwanachama kwenye akaunti ya chama, itabidi wanachama wachukue mali yoyote ya mtuhumiwa ambayo anayo nyumbani kufidia kiasi cha fedha kilichoibiwa na mtuhumiwa ashitakiwe mahakamani.

9)   WAJIBU WA MWANACHAMA
a)    Kushiriki kwa kujituma katika shughuli zote zinazolenga kufanikisha madhumuni ya Chama;
b)   Kutekeleza kwa uadilifu na nidhamu majukumu atakayopangiwa katika kutekeleza madhumuni ya Chama;
c)    Kulipa ada ya kila mwezi shilingi 10,000/=;
d)    Kuchanga fedha za rambirambi zisizopungua shilingi 10,000/= kila tukio; na
e)    Kumchangia mwanachama anayeoa/olewa kiasi kisichopungua shilingi 10,000/= (elfu kumi).

10)       UENDESHAJI WA SHUGHULI ZA CHAMA
Shughuli za chama zitaendeshwa na viongozi wafuatao:
a)    Mwenyekiti;
b)   Makamu Mwenyekiti;
c)    Katibu;
d)    Katibu Msaidizi; na
e)    Mweka Hazina.

Ili viongozi waweze kutekeleza majukumu yao kikamilifu, kutakuwa na Kamati zifuatazo ambazo zitawasaidia viongozi hao kutekeleza majukumu yao kikamilifu:

a)    Kamati ya Utendaji (wajumbe 17);
b)   Kamati ya Nidhamu na Usalama (wajumbe 5); na
c)    Kamati ya Matukio (wajumbe 7).

MAJUKUMU YA KAMATI MBALIMBALI ZA CHAMA
a)   Majukumu ya Kamati Kuu ya Utendaji
Kwa ujumla, Kamati Kuu ya Utendaji ni uongozi, yaani inaongozwa na Mwenyekiti; Mwenyekiti Msaidizi; Katibu; Katibu Msaidizi; na Mtunza Hazina. Majukumu ya Kamati hii yatahusu uendeshaji, usimammizi na uratibu wa shughuli za kila siku za Chama ikiwa ni pamoja na:
(i)   Kutunza fedha na mali zote za Chama;
(ii)  Kutunza shughuli za Chama na kumbukumbu za wanachama;
(iii)Kuandaa ratiba za mikutano na vikao vyote vya Chama;
(iv)Kusimamia utekelezaji na marekebisho ya Katiba;
(v)  Kubuni na kusimamia mikakati ya kuendeleza Chama; na
(vi)Kusimamia utekelezaji wa maamuzi ya wanachama.
10.1      Katika hali ya kawaida kamati ya utendaji itakutana mara moja kwa mwezi. 
10.2      Mkutano utaendeshwa na Mwenyekiti, kama hayupo Makamu Mwenyekiti atachukua nafasi yake.Iwapo wote hawatakuwepo basi madaraka yao yataachwa kwa mmoja wa wajumbe  wa Kamati Kuu ya Utendaji kuongoza kikao kwa niaba yao.
10.3      Endapo Katibu na Katibu Msadizi hawatakuwepo wajumbe watamchagua mjumbe mmoja kukaimu nafasi hiyo.
10.4      Wajumbe katika kamati hii watakaa madarakani kwa kipindi cha miaka mitatu (3).

11) MAJUKUMU YA VIONGOZI WA CHAMA

Kazi za Mwenyekiti
(i)   Kiongozi mkuu wa chama;
(ii)  Ataongoza mikutano yote ya chama;
(iii) Kutoa miongozo ya utekelezaji wa majukumu mbalimbali kwa mujibu wa taratibu za chama;
(iv) Kuratibu mipango ya chama na kuidhinisha matumizi ya fedha za chama kwa mujibu wa taratibu za chama; na
(v)  Atawajibika kwa mkutano mkuu wa chama.
Kazi za Mwenyekiti Msaidizi
(i)   Atakuwa msaidizi na mshauri mkuu wa mwenyekiti;
(ii)  Atafanya kazi zote atakazopangiwa na mwenyekiti; na
(iii) Atawajibika kwa mwenyekiti.
Kazi za Katibu
(i)   Atakuwa ndiye mtendaji mkuu wa chama;
(ii)  Atawajibika kwa mwenyekiti na Kamati ya utendaji;
(iii) Kuitisha na kuandaa agenda na kumbukumbu za mikutano;
(iv) Kupokea maombi ya wanachama wapya na kuwasilisha kwa Kamati Kuu ya Utendaji ili kupitishwa;
(v)  Kutunza Daftari la majina ya wanachama; na
(vi) Kupokea hoja mbalimbali za wanachama na kuzifanyia kazi.
Kazi za Katibu Msaidizi
Atafanya kazi zote atakazopangiwa na Katibu.
Kazi za Mweka Hazina
(i)   Kukusanya michango, kutunza fedha na kumbukumbu zake;
(ii)  Kutoa taarifa ya mapato na matumizi ya fedha za wanachama kwenye mikutano yote ya chama na kuhakikisha fedha zote zimepelekwa benki;
(iii) Kuandaa benki statement;
(iv) Atawajibika kwa Kamati Kuu ya Utendaji na Mkutano Mkuu wa Chama;
(v)  Kuandaa orodha ya wadaiwa kila mwezi na kuwasilisha kwenye mkutano wa wanachama wote kupitia Kamati ya Utendaji;
(vi) Kutoa ushauri wa masuala yote ya fedha kwa wanachama na namna nzuri itakayosaidia fedha kupatikana wakati wote zitakapohitajika;
(vii)                Atawajibika katika shughuli zote za kifedha na zingine atakazopangiwa na mwenyekiti.

b)   Majukumu ya Kamati ya Nidhamu na Usalama ni kufuatilia mwenendo, nidhamu na utekelezaji wa shughuli zote za chama na mwanachama.

c)    Majukumu ya Kamati ya Matukio ni pamoja na kufuatilia kwa karibu matukio yote ambayo yatawapata wanachama na kutoa taarifa haraka kwa viongozi na wanachama kwa hatua zaidi za msaada.


12)       MKUTANO MKUU WA CHAMA.
Kutakuwa na mkutano wa wanachama wote kila baada ya miezi mitatu kuanzia Januari ya kila mwaka. Mkutano wa Wanachama wote utahusika na mambo yafutayo.
a)    Kuchagua viongozi wa Chama iwapo muda umekwisha;
b)   Kuchambua mapendekezo ya Kamati Kuu ya Utendaji kuhusu mwelekeo wa Chama kwa mwaka;
c)    Kurekebisha vipengele vya katiba kwa kadri ya mahitaji ya nyakati; na
d)    Kupokea, kuchambua na kuidhinisha taarifa ya mapato na matumizi ya Chama kwa mwaka.

Ili kufanikisha mikutano ya Chama kufanyika kama itakavyopangwa, kuanzia asilimia 50 ya wanachama wote watakaohudhuria pamoja na wale waliotoa udhuru inatosha kufungua na kuendesha mkutano. Aidha, vikao vya wanachama vitaamuliwa kidemokrasia kwa kupiga kura na hoja zote lazima zipitishwe kwa zaidi ya asilimia 50 ya wajumbe wote watakaohudhuria kikao husika.

13)       MFUMO WA UENDESHAJI CHAMA
Wanachama kwa kiasi kikubwa watatekeleza shughuli zao kwa kujitolea na kujituma. Hata hivyo, wanachama watagharamia yafuatayo:-
a)    Uchapishaji wa miniti za mikutano ya wanachama, kamati ya utendaji na  mkutano mkuu; na
b)   Vifaa vya msingi vya uendeshaji wa Chama.

14)       WAKAGUZI WA HESABU
a)    Kamati ya Nidhamu na Usalama ndio itafanya shughuli zote za ukaguzi wa hesabu kila baada ya miezi mitatu (3);
b)   Kamati hii itakuwa na jumla ya wajumbe watano (5); na
c)    Nakala za mapato na matumizi pamoja na taarifa za wakaguzi wa fedha zitawasilishwa kwenye Mkutano Mkuu na zinaweza kupatikana au kuwekwa bayana kwa wanachama wote watakaozihitaji kuziona wakati wowote.

15)       MATUMIZI YA MICHANGO
a)    Endapo mwanachama (mume au mke) amefariki, Mfuko wa Chama utatoa shilingi 300,000/= (laki tatu) ili kumpa mfiwa mkuu na pia kila mwanachama atachangia shilingi zisizopungua 10,000/= (elfu kumi tu) ili kumpa mfiwa mkuu;
b)   Endapo mwanachama amefiwa na mtegemezi wake (Aya Na. 16), Mfuko wa Chama utatoa shilingi 200,000/= (laki mbili) ili kumpa mfiwa mkuu, na pia kila mwanachama atamchangia mfiwa mkuu shilingi zisizopungua 10,000/= (elfu kumi); 
c)    Endapo kwa tukio baya mwanachama atakuwa amefariki, familia yake itakuwa na hiari ya kumchagua mrithi wa hisa za marehemu au uanachama, bila kujaza fomu upya ya maombi ya uanachama;
d)    Ikiwa kutakuwa na ndugu zaidi ya mmoja katika Chama na ikatokea wamepatwa na msiba, basi Chama kitatoa msaada wa watu wawili tu wa familia hiyo ambao watawachagua kupokea msaada huo. Na katika hao ndugu, endapo mmoja wao amefiwa na mkwe wake, basi atakayepata msaada wa Chama ni mlengwa mwenyewe tu na Chama hakitawajibika kutoa msaada zaidi ya mwanachama mmoja;
e)    Gharama za vikao zitagharamiwa na wanachama wenyewe, vikao vitafanyika sehemu yoyote itakayopendekezwa na wanachama;
f)     Kuchangia katika shughuli za maendeleo ya jamii ya Nkungi na Vijiji Jirani, kutategemea aina ya msaada unaohitajika na uwezo wa Chama; Aidha, kiasi halisi cha mchango kitapitishwa rasmi na Mkutano Mkuu wa Chama. Ili kutekeleza azma hii, Chama kitaanzisha mfumo rasmi wa mawasiliano na viongozi wa Nkungi na Vijiji Jirani ili michango hiyo iweze kuwafikia walengwa kwa wakati.

16)       WATEGEMEZI WANAOSTAHILI KUHUDUMIWA NA CHAMA
Wategemezi wa mwanachama (Mume/Mke) ni hawa wafuatao:

a)    Baba/Mama mzazi wa Mwanachama;
b)   Wakwe wa pande zote mbili za Mwanachama;
c)    Watoto rasmi wa mwanachama wasiozidi wanne;
d)    Aidha, mume mwenye wake zaidi ya mmoja, ni mke rasmi mmoja tu atahesabika kuhudumiwa na chama; na
e)    Mwanaume au mwanamke ambaye hajaoa/hajaolewa atahesabika kama mwanachama mmoja.

17)       UKOMO WA UONGOZI
Kiongozi anaweza kuondolewa uongozi wake kwa:
a)    Kutotimiza masharti ya uanachama;
b)   Kutohudhuria mikutano mitatu mfululizo bila taarifa;
c)    Kujiuzulu yeye mwenyewe kwa kuacha uanachama; na
d)    Kifo.

18)       KUKOMA UANACHAMA
a)    Kwa ridhaa yake mwenyewe kwa kutoa taarifa ya maandishi/maelezo mbele ya mkutano wa wanachama;
b)   Kwa kutotimiza masharti na taratibu za Chama;
c)    Kutoshiriki katika mikutano mitatu mfululizo ya chama bila taarifa;
d)    Utovu wa nidhamu kwa wanachama wengine;
e)    Kutolipa ada ya kila mwezi kwa miezi mitatu mfululizo na pia kutolipa michango mingine mfululizo kwa miezi mitatu bila taarifa kwa uongozi;
f)     Endapo mwanachama ameshindwa kutimiza masharti yote ya uanachama (Aya Na 9, 17, 18-c,d,&e), Chama kitalazimika kumfukuza uanachama bila kurejeshewa hisa zake; na
g)    Kwa kufariki.


19)       KUHAMA KWA WANACHAMA
a)    Endapo mwanachama atahama kwenda mkoa mwingine kikazi/kuishi, atarudishiwa michango yake lakini atakatwa asilimia 50 ya akiba yake ili fedha zitakazobaki ziendeshe shughuli za wanachama waliobaki;
b)   Endapo mwanachama atahama kwenda mkoa mwingine kikazi na kuamua kuendelea kuwa mwanachama hai, kipengele 17 (b) na 18 (c) havitamhusu na atatakiwa kutimiza masharti mengine yote ya uanachama.

20)       MABADILIKO YA KATIBA
Katiba inaweza kufanyiwa marekebisho kwa kupitishwa na zaidi ya asilimia 50 ya wanachama wote.

21)       KUVUNJIKA KWA CHAMA
a)    Chama kinaweza kuvunjika endapo ni dhahiri hakuna maelewano na zaidi ya asilimia 50 ya wajumbe wamedhamiria kukivunja chama;
b)   Maamuzi ya kuvunja Chama sharti yaafikiwe na Mkutano Mkuu wa Chama kwa kuzingatia Kanuni za Chama; na
c)    Mgawanyo wa michango utafanyika kwa kuzingatia hisa pamoja na michango mingine ambayo alichangia mwanachama.


ILIANDALIWA RASMI MWEZI AGOSTI 2012

DAR ES SALAAM, TANZANIA.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni